Stori: Musa mateja/Risasi
STAA aliyewahi kukamata vilivyo kwenye anga ya muziki wa Bongo Fleva, Shabani Ramadhani ‘Matonya’ ameibuka na kumvaa mwanadada Judith Wambura ‘Jide au Lady Jaydee’ akidai amemdhalilisha kwa mashabiki wake

Akizungumza na mwanahabari wetu, Matonya alisema anamtafuta Jide popote alipo ili amuulize kinaga ubaga kwa nini aliamua kuposti picha kwenye mitandao yake ya kijamii ikimuonesha akiwa hajitambui pasipo kumtaarifu.

“Nimeumizwa sana na Jide kwa kitendo chake cha kuamua kunidhalilisha kwa kiasi hicho tena akijua mimi ni mwanamuziki mwenzake na kama kuna kitu aliona simfurahishi kwenye mwenendo wa maisha yangu basi alikuwa wazi kuniita na kunikalisha chini na siyo kama uamuzi alioutumia wa kunianika kwenye mitandao,” alisema Matonya.

Matonya alifafanua kuwa picha hiyo alipigwa katika video yake mpya lakini Jide akaichukua na kuiweka mitandaoni pasipo kumuuliza.




“Ile picha aliyoitumia kunidhalilisha ilikuwa ni ya video yangu ya wimbo mpya unaoitwa Homa ya Jiji ambayo itatoka hivi karibuni, sasa yeye ameweka mitandaoni na kusababisha watu wanidharau kwa kuona nimelewa chakari, asiponiomba radhi nitahakikisha namfikisha mahakamani,” alisema Matonya.

Kupitia ukurasa wake wa Facebook, Jide aliiposti picha ya Matonya akiwa amelala na kusindikiza na ujumbe ulioonesha kama hamjui msanii huyo hali iliyosababisha mashabiki wengi kumsema vibaya Matonya.

Post a Comment

 
Top