Waziri wa Nishati na Madini Prof Sospeter Muhongo
---
Sakata la uchotwaji wa fedha katika Akaunti ya Tegeta Escrow linaendelea kuchukua sura mpya baada ya Waziri wa Nishati na Madini, Prof Sospeter Muhongo kutoa ufafanuzi wa Serikali bungeni mjini Dodoma kuwa fedha hizo si za umma na kwamba bado Serikali ina mzigo wa madeni katika sakata hilo.



Kauli ya Prof Muhongo inakuja siku moja baada ya Kamati ya PAC kuwasilisha ripoti yake jana juu ya suala hilo ambapo pamoja na mambo mengine, Kamati ya PAC ilijiridhisha kuwa sehemu ya fedha hizo ni za Serikali.





Mwenyekiti wa PAC, Zitto Kabwe akisoma taarifa ya kamati hiyo jana alisema Kaimu Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Francis Mwakapalila, Kamishna Mkuu wa TRA, Rished Bade wakithibitisha kuwa sehemu ya fedha zilizokuwamo kwenye Akaunti ya Tegeta Escrow zilikuwa za Serikali.



Akiwasilisha maelezo ya Serikali leo, Prof Muhongo alipangua hoja moja baada ya nyingine zilizotolewa na Kamati ya PAC jana na kusisitiza kuwa fedha hizo si mali ya umma.



Prof Muhongo pia alitumia muda mwingi kueleza jinsi Kampuni ya uwakili ya Mkono and Advocates iliyokuwa ikiitetea Serikali pamoja na Tanesco, ilivyochota kiasi kikubwa cha pesa kama malipo ya kazi hiyo tangu kuanza kwa mgogoro huo.



“Gharama za mawakili; Kampuni ya Mkono & Advocates waliokuwa wakiitetea Tanesco na Serikali katika suala la IPTL tangu mwaka 1998 hadi 2013 ni Sh62.90 bilioni na bado wanaidai Serikali $ milioni nne,” alismea Prof Muhongo.



Aliongeza kuwa Kampuni hiyo ya Mkono & Advocates iliishauri Serikali kuwapa kazi nyingine ya kwenda kuitetea Serikali juu ya mgogoro huo, lakini Serikali ilikataa na kuongeza kuwa waliokoa Sh95 bilioni kwa uamuzi huo kwani uwezekano wa kushinda ulikuwa mdogo.


Credits hakingowi.com

Post a Comment

 
Top