Jeshi la polisi mkoani Arusha
linamsaka msanii wa kizazi
kipya wa jijini Dar es Salaam,
Nasibu Abdul Juma maarufu
Diamond Platinumz kwa
tuhuma za utapeli wa kujipatia kiasi cha Sh. milioni
1.5 na kushindwa kuhudhuria
shoo jijini Arusha, jambo
lililopelekea mashabiki
kufanya vurugu na uharibifu
mkubwa wa mali katika ukumbi maarufu wa Triple A. Diamond anadaiwa kuingia
mkataba na kampuni ya
Arbab MB Entertaiment ya
jijini Tanga kuja kufanya shoo
ya siku moja jijini hapa
Ijumaa Oktoba 8 mwaka huu, baada ya kukubaliana
kulipwa Sh. milioni 2.5. Hata hivyo, msanii huyo
hakuhudhuria shoo hiyo kwa
kile kinachodaiwa kuwa ni
kutokana na kuachwa na
ndege, hatua ambayo
ilisababisha vurugu kubwa katika ukumbi huo, kutoka
kwa mashabiki waliokuwa
wakitaka kurudishiwa
kiingilio, ambapo katika
vurugu hizo wacheza shoo
wa msanii huyo na mwandaaji wa shoo huyo
walitiwa mbaroni na polisi. Taarifa zaidi zimeeleza
kwamba msanii huyo alilipwa
kiasi cha shilingi milioni 1.5 na
kukatiwa tiketi ya ndege ya
kwenda na kurudi yenye
thamani ya Sh. 350,000 ambapo aliwatanguliza
wacheza shoo wake wanane
jijini Arusha. Mkurugenzi wa kampuni
Arbab iliyoandaa onyesho
hilo, Mbwana Imamu alisema
kuwa Diamond alishindwa
kutokea na hakuwa ametoa
taarifa yoyote ya kutofika kwake kwenye shoo hiyo na
kwamba muda wote
walipokuwa wakiwasiliana
kabla alikuwa akiwaambia
anakuja. Ilipofika usiku wa manane
bila msanii huyo kutokea,
zaidi ya mashabiki 2,000
waliokuwa wametoa kiingilio
(Sh. 10,000 kwa kila moja)
walianza kuleta fujo wakishinikiza kurudishiwa
fedha zao, na wakavunja viti,
chupa, glasi, vioo, samani
mbalimbali za ndani na watu
kupigwa wakiwemo maDJ
waliokuwa wakichezesha muziki. Hata hivyo, polisi waliarifiwa
na kufika katika eneo hilo
ambapo walimtia mbaroni
muandaaji wa shoo hiyo,
pamoja na wacheza shoo
wanne kati ya wanane wa Diamond ambao bado
wanashikiliwa katika kituo
kikuu cha polisi mjini hapa
huku polisi ikimtaka msanii
huyo ajisalimishe kituoni
hapo. Kwa mujibu wa mkurugenzi
wa The Blue Triple A, Papa
King, hasara iliyopatikana
kutokana na vurugu hizo ni
Sh. milioni 3.5 na kwamba
imetia doa ukumbi huo unaoheshimika hapa nchini na
Afrika Mashariki. Mbwana alisema kuwa msanii
huyo amempa hasara ya Sh.
milioni 20 ambazo anamtaka
kuzirudisha yakiwemo
malipo ya uharibifu wa
ukumbi huo. Diamond alipotafutwa kwa njia ya
simu alisema kuwa
hakufanya makusudi
kutohudhuria shoo hiyo lakini
aliachwa na ndege iliyokuwa
iondoke saa 12:00 jioni katika Uwanja wa Ndege wa
Kimataifa wa Julius Nyerere,
Oktoba 8. Hata hivyo, Diamond alisema
kuwa yupo tayari kufanya
shoo yoyote bure katika
ukumbi huo ili kufidia hasara
iliyotokea. Kaimu Kamanda wa Polisi
mkoa wa Arusha, Akili
Mpwapwa alithibitisha
kutokea kwa tukio hilo na
kusema kuwa bado
wanawashikilia wacheza shoo wanne wa msanii huyo na
Diamond anatakiwa
kujisalimisha katika kituo cha
polisi jijini Arusha.

Post a Comment

 
Top